Ungana nasi kwa kuandika email yako hapa ili upate habari mpya kupitia email yako bila usumbufu:


Home » » Mwenyekiti wa CCM aliyeuawa na wananchi mkoani mwanza atazikwa leo

Mwenyekiti wa CCM aliyeuawa na wananchi mkoani mwanza atazikwa leo

tangazo

MWILI wa Mwenyekiti wa zamani wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Mwanza, Clement Mabina (65) unatarajiwa kuzikwa leo katika eneo la Kanyama, jirani na yalipotokea mauaji yake.  Marehemu Mabina alifariki dunia Jumapili iliyopita baada ya kutokea vurugu kubwa baina yake na wananchi wa kitongoji cha Kanyama kilichopo katika Kata la Ilemela, ambayo alikuwa Diwani wake.
 

Kabla ya kufariki marehemu Mabina alimuua mtoto Natanael Malemi (12) ambaye inadaiwa alifika katika eneo la tukio baada ya kusikia kelele za wananchi waliokuwa wakimfukuza marehemu Mabina.
 

Hata hivyo inadaiwa marehemu Mabina alimfyatulia mtoto risasi iliyompiga jichoni na kutokea kisogoni baada ya kuwaonyesha wananchi alipokuwa amejificha, lakini kwa mujibu wa mama mzazi wa marehemu Juliana Natanael (40), alisema mtoto wake alikuwa amekwenda kushuhudia tukio ndipo alipopatwa na mkasa huo.
 

Chanzo cha mauaji hayo ni eneo lililokuwa likigombaniwa na wanakijiji pamoja na Mabina ambaye pia alikuwa Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi(CCM) Mkoa wa Mwanza kati ya 2007/ 2012 kabla ya kushindwa na Dk. Anthony Diallo ambaye ndiye Mwenyekiti wa sasa.
 

Baadhi ya wananchi waliozungumza na Rai walisema eneo hilo lilikuwa na mgogoro kwa muda mrefu kutokana na Mabina kushindwa kutekeleza makubaliano na wananchi hao yakiwamo ya kuwachimbia visima kwanza kabla ya kumpa ridhaa ya kumiliki eneo hilo.
 

Mwaka jana marehemu akiwa Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Mwanza pia alinusurika kupigwa na wananchi hao alipofika akiwa ndani ya gari laCCM lenye namba za usajili T491 AUP, ambalo hutumiwa na Mwenyekiti wa Mkoa.
 

Vyanzo vya habari vimesema mgogoro huo umekuwapo kwa zaidi ya miaka zaidi ya mitano na ulikuwa ukiibuka na kufifia, ambapo pia kuna taarifa mgogoro huo uliwahi kufikishwa serikalini pamoja na CCM kwa ajili ya kupatiwa ufumbuzi, lakini hakuna hatua yoyote iliyochukuliwa.
 

***Marehemu Mabina alikuwa nani?

Marehemu Clement Mabina alikuwa mfanyabiashara tangu akiwa kijana, alikuwa akifanya biashara zake baina ya Tanzania na Kenya hasa wakati ule wa uhaba wa bia nchini, ambapo alikuwa akisafirisha bia kutoka Kenya na kuziingiza nchini.
 

Baada ya kufunguliwa kwa viwanda kadhaa vya bia chini, Mabina aliamua kubadili biashara na kujikuita zaidi katika kilimo, ufugaji pamoja na kuamua kujihusisha na siasa hasa baada ya kuruhusiwa kwa mfumo wa vyama vingi vya siasa mwanzoni mwa miaka ya 1990.
 

Marehemu Mabina kwa mara ya kwanza aligombea ubunge katika Jimbo la Magu mwaka 1995 kupitia chama cha NCCR-Mageuzi, lakini kura hazikutosha na kushindwa katika uchaguzi na mgombea wa CCM wakati huo, Ernest Nyanda.
 

Baada ya kushindwa katika uchaguzi huo mwishoni mwa miaka ya 1990, Mabina aliamua kujitoa NCCR-Mageuzi na kuhamia CCM, ambapo mwaka 2000 aligombea nafasi ya udiwani katika Kata ya Kisesa wilayani Magu na kufanikiwa kushinda kwa kishindo.
 

Baada ya kufanikiwa kushinda kiti hicho, mwaka huo pia alifanikiwa kuchaguliwa kuwa Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Magu na kisha Mwenyekiti wa Jumuiya ya Serikali ya Mitaa(ALAT) Mkoa wa Mwanza.
 

Nyota yake iliendelea kung’ara katika siasa baada ya kuchaguliwa kuwa Kamanda wa Vijana wa Kata ya Magu, Mjumbe wa Bodi ya Chama Kikuu cha Ushirika Mkoa wa Mwanza (NYANZA).
 

Safari yake kisiasa iliingia dosari 2010 baada ya Kamati ya Siasa Mkoa wa Mwanza kumuwekea ngumu kuendelea na nafasi hiyo kwa kutokea vurugu baina yake na aliyekuwa Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya hiyo wakati huo, Jane Mutagurwa pamoja na baadhi ya madiwani wa Halmashauri hiyo.
 

Mwaka 2007 Mabina alifanikiwa kugombea nafasi ya Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Mwanza, na kufanikiwa kuchaguliwa baada ya kuwashinda wagombea wengine wawili.
 

Alikalia kiti hicho kwa kipindi cha miaka mitano pekee, kwani mwaka 2012 alipoteza kiti hicho baada ya kushindwa na Dk. Diallo.
 
-Mtanzania
TUPE MAONI YAKO
KAMA UMEGUSWA NA HUDUMA ZETU, TUNAOMBA UUNGANE NASI KATIKA PAGE YETU YA FACEBOOK HAPO CHINI. BOFYA "LIKE" KAMA BADO HUJA LIKE PAGE YETU.
KUMBUKA KU LIKE UKURASA WETU WA FACEBOOK
 
Support : mpekuzi | John mpekuzi | Wataalam
Copyright © 2009. DOMO LANGU - All Rights Reserved
Template designed by mpekuzi
Proudly powered by Blogger